| dc.description.abstract |
Wataalam waliohusika na utafiti wa lugha wanabaini kwamba lugha ya kwanza
inaathiri ujifunzaji wa lugha ya pili, na hivyo kumletea mjifunzaji wa lugha ya pili
changamoto mbalimbali. Huu utafiti ulichunguza namna sarufi ya lugha ya Kinyankore
inavyoathiri ujifunzaji wa Kiswahili. Aidha, ulilenga kubaini changamoto
zinazowakabili wanafunzi wa Kinyankore wanapojifunza Kiswahili kama lugha ya pili,
na mwisho, kutoa mapendekezo ya jinsi ya kushughulikia changamoto hizo. Huu utafiti
ulikuwa na malengo maalum matatu: Kwanza, kubaini athari za Kinyankore na vile
zinavyojitokeza wakati wa kusoma somo la Kiswahili ikiwa ni lugha nyingine. Pili,
kuchunguza kwa nini athari hizo zinajitokeza kwa wanafunzi hao wa Kinyankore
wakati wanapojifunza lugha hiyo nyingine ya Kiswahili. Lengo la tatu lilikuwa
kutambua mbinu mbalimbali zinazotumika kukabiliana na changamoto hizo na
kusaidia wanafunzi waathiriwa wa Kinyankore katika mchakato wa kujifunza
Kiswahili. Mahali ambapo utafiti huu ulifanyika ni jijini Mbarara katika asasi za elimu
zilizochaguliwa, na mtafiti alilenga asasi teule za shule za sekondari na Vyuo vikuu.
Takwimu za utafiti zilipatikana baada ya kuhusisha njia mbalimbali za ukusanyaji wa
data, kama vile mahojiano, majadiliano, mazungumzo, hojaji, pamoja na dodoso. Njia
ya usampulishaji maalum na nasibu zilitumika kuteua washiriki waliochaguliwa. Jumla
ya washiriki katika utafiti huu ilikuwa mia mbili (200). Utafiti huu ulilenga kutumia
idadi hii ya washiriki ili kupata maoni yanayowakilisha kundi kubwa zaidi mkoani.
Utafiti huu ulichochewa na nadharia mseto, ambayo inajumuisha nadharia kadhaa hasa
ile ya Uchanganuzi Makosa, Nadharia ya Uchanganuzi-Linganuzi, pamoja na ile ya
Mawasiliano. Aidha, utafiti ulifanikiwa kubainisha mbinu zinazotumika kuwasaidia
wanafunzi wanaokabiliwa na taathira za sarufi ya Kinyankore wakijifunza Kiswahili.
Utafiti ulibainisha kwamba wanafunzi wa Kinyankore wanakabiliwa na changamoto za
kisarufi katika ujifunzaji wao wa Kiswahili katika nyanja za kimsamiati, kifonolojia,
kimofolojia, kisemantiki na kimuundo. Utafiti ulionyesha kwamba wanafunzi
wanakabiliwa na matatizo kadhaa ya kiisimu, mkiwemo matatizo ya kisarufi,
kimaandishi, kuchanganya ndimi pamoja na changamoto katika kutafsiri vipengele vya
Kiswahili kulingana na lugha ya Kinyankore. Kuhusu lengo la pili, utafiti ulitambua
sababu za sarufi ya kinyankore kuathiri namna Kiswahili kinavyosomwa kwa
kuzingatia vigezo vyote vya sarufi ya lugha ya kwanza, matumizi ya ala za sauti za kaa
kaa, kukosekana kwa baadhi ya fonimu katika kinyankore, kufundisha vibaya kwa
somo la Swahili, mazingira yasiyofaa kujifunzia somo la Kiswahili, nakadhalika.
Kulingana na lengo la tatu, utafiti ulionyesha mbinu zinazotumika kukabiliana na
changamoto za wanafunzi wenye asili ya Kinyankore wanapokuwa katika mafunzo ya
Kiswahili. Na hizo mbinu ni pamoja na; kufundisha Kiswahili tangu utotoni, wanafunzi
wa kinyankore wapewe nafasi za matumizi na mazungumzo ya Kiswahili, kuhamasisha
wazazi, walimu na wanafunzi kuhusu umuhimu wa Kiswahili, kuongeza vipindi na
muda wa kufundisha Kiswahili kwenye ratiba za shule, kuweka mazingira rafiki ya
kujifunzia Kiswahili na kadhalika. Utafiti ulihitimisha kwamba, ijapo Kinyankore
kinaathiri kujifunza somo la Kiswahili kwenye ngazi zote za kisarufi kisarufi kama vile
kimatamshi, kisemantiki, kimsamiati, kimuundo na kimofolojia, athari hizo haziwezi
kuzuia mafunzo ya somo la Kiswahili kuendelea. Kwa maana, Kinyankore jinsi
inavyotambulika kuwa Kibantu huenda ikasaidia wanafunzi kutumia uwezo wao
kuelewa jinsi matumizi na uundaji wa maneno ya lugha ya Kiswahili yanavyojitokeza.
Utafiti ulihitimisha kwa kupendekeza kwa tafiti zijazo kutumia nadharia nyingine
kuchunguza athari zinazojitokeza katika ujifunzaji wa lugha ya pili, pamoja na kutumia
muda mwingi zaidi kuzibainisha sababu na suluhisho za kila moja. |
en_US |